love and relation

Upendo wa Kweli Haupo Kwenye Tendo Pekee!


Utafiti unaonesha kuwa, hali hii ipo zaidi kwa vijana wa sasa ambao tendo la ndoa kwao limekuwa kama sehemu ya maisha yao.

Kila wanapokuwa wanawaza tendo hilo tu, hawana muda wa kujadili mambo mengine ya maendeleo zaidi ya mapenzi. Kibaya zaidi wanasahau kuwa mapenzi wanayoyapenda na kuyajadili muda wote yanahitaji kustawishwa kwa fedha, kwa maana ya kumtunza na kumpendezesha mpenzi wako.

Mada hii inazungumzia upendo wa kweli kwa wapenzi kuwa, haupo kwenye kufanya tendo la ndoa au kwa wanandoa bali upo kwenye mambo mengi sana kama vile;

KUHESHIMIANA

Kwa mtu anayempenda kwa dhati mpenzi au mwandani wake ni lazima atamheshimu, atamtunzia heshima yake popote aendako. Hata kama kuna watu wanamsema kwa mabaya ya kweli lakini yeye atajitahidi kutumia nguvu na ushawishi mwingi ili kumfichia ubaya mpenzi wake.

KUVUMILIANA

Changamoto za maisha kwa wapenzi huwa ni nyingi lakini kwa umpendaye, upendo wa kweli unanakshiwa na uvumilivu.

KUTHAMINIANA

Kuwa tayari kusikiliza shida za mwenza wako na kuzitatua hata kama huna uwezo wa kuzitatua, lakini kauli na maneno yako yanaonesha unaweza. Kauli ambazo zinamridhisha mpenzi wako na kumfanya aamini kuwa kuna siku utatimiza kile ulichokusudia kwake.

KUMPENDEZESHA

Kama kweli unampenda kwa dhati mpenzi wako ni lazima utahakikisha unampendezesha kwa kila namna ili kila siku aendelee kuonekana mzuri na bora machoni pako na kwa wengine.

KUELEWANA

Wenye mapenzi ya kweli muda mwingi huelewana, hata kama watatibuana lakini muda mchache tu wanaelewana na unakuta wanafanya kitu ambacho huwezi kuamini kama waligombana au kutukanana.

KULINDANA

Mpenzi unayempenda utamlinda kwa namna yoyote ile, hauko tayari kuona akionewa, akilia, akitukanwa, akipigwa na mambo mengine kama hayo. Unamlinda hata katika kujali afya yake. Lakini wapenzi wengi wa sasa wamegeuza mapenzi ndiyo kila kitu kwao, vitu vingine havina nafasi katika uhusiano zaidi ya mapenzi.

Ingawa tendo la ndoa ndiyo hasa kiunganishi kikubwa cha wapenzi, lakini mapenzi pekee hayatoshi kukamilisha upendo wa dhati kwa wapendanao.